Рет қаралды 50,490
Yalikuwa ni mauaji ya kikatili, ndivyo unaweza kuelezea mauaji ya askari watatu wa Jeshi la Polisi waliokuwa lindo katika benki ya CRDB jijini Dar es Salaam, kuuawa kwa kupigwa risasi na kuporwa bunduki mbili, ikiwamo AK-47.
Ni kutokana na mauaji hayo yaliyotokea katika eneo la benki ya CRDB Mbande katika wilaya ya Ilala, Januari 30, 2025 mahakama imemtia hatiani Mbwana Suleiman Puga, na kumhukumu adhabu ya kunyongwa hadi kufa.
Hukumu hiyo iliyohusu mauaji hayo yaliyotokea Agosti 23, 2016 ilitolewa na Jaji Hussein Mtembwa wa Mahakama Kuu kanda ya Dar es Salaam, ambaye alisema mikono yake imefungwa na kiapo alichoapa kulinda Katiba na sheria za nchi, hivyo anamhukumu adhabu stahiki ya kifo kwa kosa hilo.
Maelezo ya upande wa mashtaka ni kuwa siku ya tukio, polisi wawili walikuwa lindo katika benki hiyo na wakati wanakabidhiana zamu na wenzao wawili, kundi la watu wenye silaha liliwavamia kwa kuwashtukiza na kuwashambulia kwa risasi.
Katika shambulizi hilo, polisi watatu G.9996 konstebo Gaston, E.5761 Koplo Yahaya na F.4666 koplo Khatibu waliuawa papo hapo kwa risasi wakati mwenzao G.9524 Kostebo Tito alijeruhiwa vibaya na kufariki akipatiwa matibabu hospitalini.
Ilielezwa kuwa katika shambulio hilo, bunduki moja aina ya Avtomat Kalashnikov (AK-47) na nyingine aina ya Semi-Automatic Rifle (SAR) ziliporwa na watu hao.
Haikuishia hapo kwani watu hao walikwenda kituo kidogo cha polisi kilichopo jirani cha Mbande na kuiba sare za Polisi na kwa msaada wa wananchi, miili ya askari hao pamoja na aliyejeruhiwa, ilipelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).
Uchunguzi wa miili ya marehemu, ilibaini vifo vyao vilitokana na majeraha mabaya ya risasi na kupoteza damu nyingi na baada ya uchunguzi wa kina wa polisi, Mbwana Suleiman Puga alikamatwa na Polisi Agosti 11, 2017.
Ilielezwa baada ya kuhojiwa na makachero wa Jeshi la Polisi, alikiri kuhusika na tukio hilo na aliwaongoza polisi mahali alipokuwa amehifadhi bunduki mbili aina ya SAR na moja SMG, risasi 31 na waya 69 za kulipuliwa mabomu. Puga alifikishwa mahakamani na kusomewa mashtaka manne ya mauaji ya askari hao na kuyakanusha, ambapo upande wa mashtaka ukalazimika kuita mashahidi 13 na kuwasilisha vielelezo halisi na nyaraka 14 kuthibitisha mashtaka hayo.
Simulizi za mashahidi
Shahidi wa kwanza aliyepewa jina la “P” alieleza Agosti 23, 2016 saa 1:00 usiku, akiwa kituo cha polisi Mbande, alipokea simu kutoka kwa askari mwenzake aliyekuwapo zamu CRDB Mbande kuwa wameshambuliwa na watu wenye silaha.
Wakati akitoa taarifa hiyo, polisi huyo alikuwa ametoroka kutoka eneo la tukio na alikuwa amejificha mahali, ndipo alikusanya polisi wengine na kwenda eneo la tukio wakitumia gari la kiraia na alipofika alishuhudia miili ya askari watatu.
Alijulishwa pia polisi mwingine, Konstebo Tito alikuwa amejeruhiwa vibaya na alikuwa amepelekwa MNH na raia wema na hapo alimfuata polisi aliyekuwa amejificha akiwa na hofu na katika tukio hilo baya, walipoteza askari wanne.
Shahidi wa pili aliyepewa jina la “P1”, alieleza siku ya tukio, aliripoti kituo cha Polisi Mbagala na walikuwa wamepangiwa zamu CRDB Mande yeye na Koplo Hatibu na kama ilivyokuwa utaratibu, wote walichukua bunduki aina ya AK 47.
Waliingia katika gari la polisi na kwenda hadi eneo la kazi na kufika salama lakini wakiwa pale walivamiwa na kushambuliwa na watu wasiojulikana na yeye alikuwa amesimama karibu na Koplo Hatibu na muda kidogo alimuona amelala chini.
Naye alilala chini wakati anaandaa bunduki yake aina ya AK-47 ambazo hujulikana pia kama Sub Machine Gun (SMG), alibaini ilikuwa haifanyi kazi sawa sawa na wakati huo huo wauaji hao waliendelea kuwashambulia kwa mvua ya risasi.
Alifanikiwa kutoroka eneo hilo na kwenda kujificha nyumba ya jirani huku milio ya risasi ikiendelea kusikika na ndipo alipoweza kumpigia simu shahidi wa kwanza na kumjulisha nini kimetokea, na milio iliendelea kusikika na baadae ikakoma.
Alieleza baadaye shahidi wa kwanza alifika akiwa na askari wengine wakiwa na gari ya kiraia ambapo kwa pamoja walikwenda hadi eneo la tukio na kushuhudia miili ya askari wenzako watatu wakiwa wamekufa.
Shahidi wa tatu, “P2”, alieleza siku ya tukio alikuwa akitengeneza gari lake nje ya benki ya CRDB Mbande na akiwa pale, lilikuja gari la polisi aina ya Leyland Ashork namba PT 38889 likiwa na askari kwa ajili ya kulinda benki hiyo.
Alieleza polisi mmoja alishuka katika gari hiyo na alipigwa risasi na watu asiowajua na mwingine aliyeshuka katika gari hilo naye alipigwa risasi na mwingine naye aliposhuka kwenye gari naye alishambuliwa kwa risasi.
Polisi mwingine alichukua bunduki na kujaribu kufyatua risasi lakini haikufanya kazi na ndipo alipoamua kujificha na aliwashuhudia watu hao wakielekea kituo kidogo cha Polisi cha Mbande na aliporudi eneo la tukio alikuta miili mitatu.