Рет қаралды 3,386
Katika hali isiyokuwa ya kawaida, maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam leo wametapakaa askari wa Jeshi la Polisi wanaozunguka huku na kule wakiashiria kuimarisha ulinzi.
Mwananchi Digital imewashuhudia askari hao wengine wakiwa wamejitami kwa kuvaa kofia ngumu maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam, hususan eneo la Morroco jijini humo tangu saa 1:30 asubuhi ya leo Septemba 21, 2024.
Wakati baadhi ya watu wakihisi pengine doria za askari hao zina uhusiano na vuguvugu la maandalizi ya maandamano ya amani yaliyopangwa kufanywa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Septemba 23, 2024, uongozi wa jeshi hilo kanda maalumu ya Dar es Salaam, umeeleza kuwa doria hizo ni sehemu ya kawaida ya ulinzi kwa wananchi.
‘’Hali hii ni ya kawaida ya masuala ya kiusalama, kama ungekuwa unazunguka hii hali ipo, na kimsingi tunataka twende na ndio maana unasikia tunataka kwenda kwenye mfumo wa kanda. Ni mfumo wa jeshi kupeleka usalama mpaka kwenye kata,’’ amesema Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro
Chadema ilitangaza maandamano hayo Septemba 12 mwaka huu, ikiishinikiza Serikali ifanikishe kurejeshwa kwa wanachama wake kadhaa waliopotea.
Hata hivyo, baadhi ya wadau wa siasa wakizungumza katika kongamano la hali ya demokrasia nchini hivi karibuni, walieleza haja ya kuwapo kwa mazungumzo kati ya Chadema na Jeshi la Polisi.
Hata hivyo, kupitia taarifa iliyotolewa na Ofisa Habari wa Chadema Kanda ya Pwani Gerva Lyenda imesisitiza na kuwataka wanachama wake kujitokeza katika maandamano hayo yanayotarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam.
Barua hiyo ya Septemba 20,2024 inasomeka kama ifuatavyo;
“YAH: TAARIFA YA MAANDAMANO YA AMANI TAREHE 23 SEPTEMBA,2024
JINIDARES SALAAM.
Leo Ijumaa tarehe 20 Septemba,2024 Viongozi wa Chama wamewasilisha barua ya kutoa taarifa Kwa Mkuu wa Polisi Mkoa wa Ilala na Mkoa wa Kipolisi Kinondoni kutoa taarifa ya Maandamano kwa mujibu wa kifungu cha 11(4) cha Sheria ya Vyama vya Siasa toleo la mwaka 2019.
Wamejulishwa rasmi kwamba Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kitafanya maandamano ya amani siku ya Jumatatu tarehe 23 September, 2024 kuanzia saa 1:00 (saa moja asubuhi) hadi saa kumi jioni kuanzia eneo la Magomeni kupitia barabara ya Morogoro road hadi viwanja vya Mnazi Mmoja na kutoka lala Boma sokoni kupitia barabara ya uhuru Hadi viwanja vya Mnazi Mmoja.
Ujumbe wa maandamano ambao ni KUPINGA, KULAANI na kuitaka Serikali ikomeshe mara Moja wimbi la watu kutekwa,kupotezwa, kuumizwa na wengine kuuwawa kiholela nchini.
Aidha tunaitaka Serikali na Jeshi la Polisi kuwarejesha Viongozi wetu ambao wametekwa na mpaka Sasa hawajulikani walipo pamoja na amri ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar Es salaam kutoa amri Kwa Jeshi la Polisi kuwatafuta ila hakuna taarife yoyote imetolewa Kwa unina na familia kuhusu utekelezaji wa amri hiyo ya Mahakama Kuu.
Tunawakaribisha wananchi wote wajitokeze Kwa Wingi ili tuandamane Kwa Amani na kufikisha maombolezo na Kilio chetu ili Kwa pamoja tuweze kukomesha mauaji haya ya kiholela nchini, hakuna ambaye Yuko salama miongoni mwetu hivyo ni wajibu wetu sote kuungana na kupaza sauti zetu! Hata wale wanaofikiri kuwa sio wanasiasa hawako salama watoto wetu no hawako salama kwani matukio haya yamekithiri nchini.”
Siku moja baada ya kutoa kauli hiyo, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, imetoa kipeperushi kinachodai siku hiyo ya Septemba 23,2024, itakuwa ni siku ya maadhimisho ya siku ya amani Mkoa wa Dar es Salaam.
Maadhimisho hayo yatakuwa na kauli mbiu ‘Dumisha amani, Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024’