Рет қаралды 2,954
Katika hali isiyokuwa ya kawaida watu wasiofahamika wamevamia na kuvunja sanamu la Mwalimu Nyerere lililopo Mtaa wa Matola, Kata ya Chemchem Manispaa ya Tabora, ambapo wameondoka na shingo ya sanamu hilo pamoja na fimbo aliyokuwa akiishikilia Nyerere enzi za uhai wake.
Akizungumzia tukio hilo leo Jumamosi Septemba 21, 2024, Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora, Richard Abwao amesema kitendo hicho kimetokea usiku wa kuamkia leo.
Amesema wahalifu wamevunja na kuondoka na shingo ya sanamu hilo pamoja na fimbo, huku akisisitiza tayari uchunguzi kuhusu tukio hilo umeanza kufanyika.
"Tumefika hapa na kukagua eneo la tukio na ni kweli kwamba sanamu hili limeondolewa kutoka kwenye sehemu, ambayo ilikuwa imehifadhiwa kwenye mnara wake. Sanamu hili limevunjwa maeneo matatu. Kikubwa tunachunguza kujua ni mazingira gani yamesababisha sanamu lifike chini,’’ amesema.
Ameongeza: ‘’Kwenye eneo la tukio tumekuta kipande cha shuka na suruali nyeusi. Kipande cha fimbo kilichotengenezwa na zege hakipo, hivyo uchunguzi tunaofanya utatupa majibu maana changamoto ya eneo husika ni eneo ambalo halina ulinzi, pia hakuna umeme, tukio hilo limegundulika asubuhi.