Рет қаралды 63,731
Uongozi wa Kampuni ya Mabasi ya Tashriff umesema tukio la kutekwa kwa aliyekuwa kada wa Chadema, Ally Kibao ndani ya usafiri wao, liliwashtua na wamedai walishindwa kuzuia kutokana na wahusika kuwa na silaha za moto.
Pia, umedai watu hao waliwatisha wafanyakazi waliokuwa ndani ya basi hilo kwa kutumia silaha za moto, baada ya tukio hilo waliripoti Kituo cha Polisi Magufuli.
Kibao, aliyekuwa Mjumbe wa Sekretarieti ya Chadema alichukuliwa ndani ya basi hilo jioni ya Ijumaa Septemba 6, 2024, eneo la Kibo Complex, Tegeta jijini Dar es Salaam, wakati akisafiri kwenda nyumbani kwake, mkoani Tanga.
Tukio hilo lilianza kujadiliwa maeneo mbalimbali Jumamosi ya Septemba 7, 2024, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika alizungumza na waandishi wa habari kuzungumzia tukio hilo na kutoa wito kwa vyombo vya usalama kulichunguza.
Katikati ya mijadala hiyo, asubuhi ya jana Jumapili, Septemba 8, 2024, kuliripotiwa mwili wa Kibao uliokuwa umetupwa Ununio, jirani na viwanja vya NSSF na ulichukuliwa na kupelekwa Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala, Dar es Salaam.
Uchunguzi wa kitabibu ulifanyika jana hospitalini hapo na taarifa yake bado haijatoka, ingawa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliyekuwapo alidai Kibao kabla ya kufikwa na mauti aliteswa na kumwagiwa tindikali usoni.
Mwili wa Kibao unazikwa mchana wa leo saa 7 mchana mkoani Tanga. Viongozi mbalimbali wamehudhuria akiwemo Mbowe, Mnyika, Naibu katibu wakuu wa Chadema, Salum Mwalimu (Zanzibar), Benson Kigaila (Bara) na Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamad Masauni.
Leo Jumatatu, Mwananchi limezungumza na Msimamizi wa Mabasi ya Tashriff, Dar es Salaam, Shaban Shemweta ambaye amedai tukio la kuuawa kwa mzee huyo limewahuzunisha.
Amedai watu waliosimamisha basi hilo walikuwa na magari mawili yasiyo na namba ya utambuzi na baada ya kulisimamisha basi hilo, mtu mmoja alikwenda mbele ya gari na kumuamuru dereva asiliondoe gari na wengine wenye silaha kupanda ndani na kumchukua kwa nguvu wakiwa wamemfunga pingu.