Рет қаралды 6,144
Wizi uliotokea katika Hospitali ya Rufaa mkoa wa Njombe umesababisha watumishi wa Idara ya Manunuzi, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na Katibu katika Hospitali hiyo kusimamishwa kazi kupisha uchunguzi kwa muda kutokana na wizi huo wa Televisheni (TV) 15 zenye thamani ya zaidi ya shilingi za kitanzania milioni 11.7 na kompyuta 2 mali ya hospitali hiyo.
Maamuzi hayo yametolewa na Mkuu wa Mkoa wa Njombe Anthony Mtaka aliyefika katika Hospitali hiyo akiwa ameongozana na Kamati ya Usalama Mkoa baada ya kubaini wizi huo huku watuhumiwa wa kwanza wakiwa ni watumishi wa hospitali hiyo ambapo mazingira ya siku ya tukio yanaonesha kontena lililokuwa na vifaa hivyo lilifunguliwa kwa funguo.
Imeelezwa baada ya wizi huo kutokea, haikotolewa ripoti yoyote ya wizi kwenda Jeshi la Polisi badala yake walizungumza na moja ya mfanyabiashara mjini Njombe ambaye aliwakopesha TV 15 bila makubaliano ya maandishi wakiahidi kumlipa baada ya kupata fedha kupitia kuchangishana.
Watumishi hao watapisha uchunguzi utakaofanyika kwa siku saba na kisha kuandaliwa ripoti ya mkoa ili kubaini wahusika wa wizi huo.
Jeshi la Polisi mkoa huo limesema tayari limeshafungua jalada la uchunguzi la tukio hilo na pindi watakapokamilisha na kubaini wahusika watawachukulia hatua za kisheria.