Рет қаралды 8,052
Hoseni, ndugu yangu Hoseni
Hivi wakumbuka?
Ulipotamka, nia ya kuponya, taifa mulolikhini
Huku ‘mezungukwa, nao manyung’unya, wasotambuwa imani
Kundi la vibaka, wanaonyang’anya, pasi na haya usoni
Bado ukataka, muliotuwinya, nasi tuwemo kundini
Japo kwa mashaka
Miye hainuka
Nikipepesuka
Bega hakushika, kukupa nafasi, uongoze njia!?
Hoseni, mwanangu Hoseni
Bado wakumbuka?
Yale maumivu, muliyotutia, makubwa yaso kifani
Na yale makovu, yaliyotitia, yaliyozama nafusini
Kwa wenu uovu, mukazitibuwa, nyoyo za wenye hisani
Za wavumilivu, nikazichukuwa, haja nazo kiganjani
Kwa roho tulivu
Na unyenyekevu
Na kwa usikivu
Pasi utukivu, kwa yangu kauli, nikakuridhia!?
Hoseni, oo Hoseni
Bado wakumbuka?
Nilimomupita, mkongwe ningawa, nikasimama makini
Nikawafuata, watu wenye pawa, na wenye mwingi uoni
Wengine haweta, wakaitikia, wakajaa vikaoni
Wengine wakanisuta, wakanichukia, kwa mabaya kunidhani
Lakini
Kwa hatua za tata
Mbele hakuleta
Nawe ukapata
Mahaba kuvuta, mwanzo wa imani, kusafiwa nia!?
Hoseni Ali Hasani
Kumbe ukingoja:
Itaponifika, siku ya kutwawa, ya kuitwa na Manani
Wende kunizika, nilikozaliwa, Mtambwe Nyali nyumbani
Na juu ya shuka, ukayashindilia, Maridhiano dongoni
Ulipoondoka, ukaniwachia, mwenyewe mwana wa ndani
Ukayageuka
Uliyotamka
Yote ‘meyeyuka
Yote ‘metoweka, kama vile moshi, mawinguni ‘mepotea!
Hoseni ee Hoseni!
Kaa na kumbuka
Radhi kwa hakika, si mja hutowa, bali Mola Rahmani
Tuliyoandika, kwamba yatakuwa, hata kama unayakhini
Walokuzunguka, wanayabiruwa, nawe wayaponda mchangani
Juwa itazuka, mbegu maridhawa, mbegu ya yangu visheni
Mche utatoka
Mizizi itajishika
Mti utanawirika
Ikiwa si Mwaka, basi japo Vuli, matunda yatazaliwa!
MOHAMMED GHASSANI
8:00 USIKU
26 JULAI 2021
BONN
UTUNGO: Waraka wa Maalim
MSHAIRI: Mohammed Ghassani
ALA: Ally Fadhil Juma