Рет қаралды 27,455
naweza kusema siku ya kwanza ya kikao cha Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ilikuwa sawa na moto.
Kinaelezwa kuwa kilikuwa kikao cha kusemezana, kuonyana na kuambiana ukweli.
Kikao hicho kilichoanza juzi saa tano asubuhi, licha ya kuwa na ajenda kadhaa, kilishuhudia Makamu Mwenyekiti-Bara, Tundu Lissu akiwasilisha ushahidi wa kauli yake kuhusu tuhuma ya rushwa kwenye uchaguzi wa ndani wa chama hicho.
Awali, Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje wa chama hicho, John Mrema, alieleza pamoja na mambo mengine, kikao hicho kingepokea taarifa ya uchaguzi katika ngazi mbalimbali.
Pia, kupokea taarifa ya tathmini ya maandamano ya awamu ya kwanza ya mikoa katika ‘wiki ya maandamano’ na kuweka mwelekeo awamu ya pili ya maandamano.
Pia kufanya usaili na kuteua wagombea nafasi za uongozi katika kanda nne za Nyasa, Serengeti, Victoria na Magharibi.
Joto la Lissu
Hata hivyo, licha ya ajenda hizo, Mwananchi lilidokezwa kuwa kauli ya Lissu kuhusu tuhuma za rushwa, iliibua joto kikaoni.
Chanzo kutoka ndani ya chama hicho, kilieleza kuwa Lissu aliyewahi kuwa mbunge wa Singida Mashariki, aliwasilisha ushahidi wake kuhusu kauli yake aliyoitoa Mei 2, mwaka huu mkoani Iringa, akidai uwepo wa fedha zilizomwagwa kwenye uchaguzi wa ndani wa Chadema.
Katika hotuba yake siku hiyo Lissu alisema: “Wakati nakuja hapa Iringa jana na juzi kulikuwa na mtafaruku mkubwa sana, sijui kama mnafahamu, ndani ya chama chetu kuna pesa nyingi ajabu kwenye uchaguzi huu.’’
Kauli hiyo ya Lissu iliibua mjadala ndani na nje ya Chadema. Makada wa chama hicho waligawanyika wapo waliomuunga mkono na wapo waliodai inakigawa chama kuelekea uchaguzi wa kanda.
Baada ya mjadala huo kushika kasi, Mei 5, mwaka huu, alipoulizwa na gazeti hili, Lissu alisema kauli yake hiyo haina tofauti na ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliyekuwa akikemea rushwa ndani na nje ya CCM.