Рет қаралды 2,088
Wataalamu wa uchongaji na uchoraji wametaja sababu zinazoweza kufanya sanamu kushindwa kubeba mfanano wa mtu husika ikiwemo kukosekana kwa uwiano halisi na vipimo.
Mbali na kutoa sababu hizo, pia wameshangaa kuendelea kuwapo kwa sanamu ambazo hazina uhalisia, huku wakieleza kuwa hivi sasa teknolojia imerahisisha kila kitu ikiwemo utengenezaji sanamu.
Wametoa kauli hizo ikiwa ni siku moja baada ya kuzinduliwa kwa sanamu la aliyekuwa Rais wa kwanza wa Tanzania, hayati Julius Nyerere nchini Ethiopia, huku likiacha gumzo mitandaoni na watu wengi kudai kuwa sanamu hilo halifanani na hayati Nyerere.
Sanamu hilo lililozinduliwa makao makuu ya Umoja wa Afrika (AU) jijini Adis Ababa, Ethiopia limewekwa mbele ya jengo la siasa, amani na usalama la Mwalimu Julius Nyerere ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika harakati za ukombozi wa bara la Afrika na kuhimiza umoja na Amani.
Hatahivyo, Madaraka Nyerere ambaye ni mtoto wa Nyerere alipohojiwa alisema akiwa miongoni mwa wanakamati kwa ajili ya kusimamia mchakato wa utengenezaji wa sanamu hiyo, waliipitisha kwa zaidi ya asilimia 90.
Akizungumzia changamoto katika uchongaji na ufinyanzi, Mhadhiri wa chuo kikuu cha Dar es Salaam idara ya Sanaa, Digna Enock ansema makosa yanayofanyika ni wasanii kushindwa kufuata kanuni za uchongaji na ufinyangaji.